"Fiat Justitia Ruat Caelum"

UTAWALA WA SHERIA: UMUHIMU NA UIMARISHAJI WAKE NCHINI - HOTUBA YA DAG

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
OFISI YA MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI

UTAWALA WA SHERIA: UMUHIMU NA UIMARISHAJI WAKE NCHINI. HOTUBA ILIYOTOLEWA NA NDG. GEORGE M. MASAJU, NAIBU MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI, WAKATI WA MAADHIMISHO YA SIKU YA SHERIA NCHINI DAR ES SALAAM, 6 FEBRUARI, 2013

Mheshimiwa Dr. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; 

Mheshimiwa Anne Makinda, (Mb) Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; 

Mheshimiwa Mohamed Chande Othman, Jaji Mkuu wa Mahakama  ya Tanzania;

Waheshimiwa Majaji wa Mahakama ya Rufani; 

Mheshimiwa Jaji Mkuu Mstaafu Augustino Stephen Lawrence Ramadhani; Mheshimiwa Jaji Mkuu Mstaafu Barnabas Samatta; 

Mheshimiwa Mathias Chikawe, (Mb) Waziri wa Katiba na Mambo ya Sheria; Mheshimiwa Jaji Kiongozi; 

Waheshimiwa Majaji wa Mahakama Kuu; 

Waheshimiwa Majaji Wastaafu; 

Waheshimiwa Mabalozi; 

Viongozi wa Vyama vya Siasa; 

Mtendaji Mkuu wa Mahakama; 

Wastahiki Viongozi wa Dini na Madhehebu mbalimbali; 

Mheshimiwa Msajili Mkuu, Msajili wa Mahakama ya Rufani; na Mahakama Kuu; Waheshimiwa Mahakimu wa ngazi zote; 

Rais wa Chama Cha Mawakili; 

Wasomi wenzangu Mawakili; 

Mabibi na Mabwana; 

Leo tunaadhimisha Siku ya Sheria inayoashiria kuanza kwa Mwaka Mpya wa shughuli za Mahakama ya Tanzania. Shughuli za Mahakama zinajumuisha kusikiliza mashauri na kuamua kuhusu haki na wajibu wa wadai na wadaiwa au washtaki  na  washtakiwa.  Maadhimisho  haya  yanafanyika  pia  mikoani  na wilayani. Tunafarijika kuona ushiriki wa pamoja wa Wakuu wote wa Mihimili ya dola iliyotajwa katika masharti ya Ibara ya 4 ya Katiba ya Nchi katika kuizindua siku hii.    Maudhui  ya  siku  ya  sheria  Mwaka  huu  ni;  “UTAWALA  WA  SHERIA: UMUHIMU WA UIMARISHAJI WAKE NCHINI.” 

Mhe. Rais, Utawala wa sheria ni dhana inayoelezea namna mamlaka ya nchi pamoja na Serikali yanavyotekelezwa kihalali iwapo tu yanafanywa kwa kufuata sheria. Uhalali wa vyombo vyote vya Serikali pamoja na taasisi zake sharti uwe na mizizi kwenye sheria ikiwa na maana kwamba uendeshaji wa shughuli  zote  za  umma  unatokana  na  sheria  zilizotungwa  ambazo  sharti zizingatiwe na kutekelezwa ipasavyo na wananchi wote. Ndiyo maana enzi za uhai wake Mwalimu J.K.Nyerere aliwahi kutamka kwamba;

 “Serikali ni sheria. Hakuna  kitu  kinaitwa  Serikali  bila  sheria;  na  sheria  zikishatungwa  lazima zifuatwe.” 

Aidha, Katiba yetu ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania katika ibara yake ya 26 inaelekeza kwamba kila mtu ana wajibu wa kufuata na kutii Katiba hiyo na sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Na kwamba kila mtu ana haki kwa kufuata utaratibu uliowekwa na sheria kuchukua hatua za kisheria  kuhakikisha  hifadhi  ya  Katiba  na  Sheria  za  nchi.  Niongeze  tu  hapa kwamba  mtu  anayezungumzwa  hapa  ni  pamoja  na  Serikali  ambayo  kwa mujibu  wa  Katiba  yetu  hiyo  katika  Ibara  ya  4  ndiyo  yenye  mamlaka  ya  utendaji. Kwa hiyo Serikali inalo jukumu la kuhakikisha kwamba Katiba na sheria zinazotokana na Katiba hiyo zinazingatiwa na kutekelezwa ipasavyo na kila mtu nchini. 

Mhe. Rais, Dhana hii ya utawala inalenga kuzuia matumizi mabaya ya madaraka na kuweka mipaka ya mamlaka ya Serikali na taasisi zake pamoja na wananchi kuishi kwa kuzingatia sheria za nchi kwa manufaa yao kijamii kiuchumi na kisiasa.  Kwa  ujumla  utawala  wa  sheria  ni  sharti  mojawapo la kustawi kwa demokrasia, na una jukumu muhimu katika kulinda na kukuza haki za binadamu, demokrasia na utawala bora na hivyo kuchochea maendeleo ya nchi. 
Baadhi ya nguzo muhimu katika utawala wa sheria ni pamoja na: 

(i) Mgawanyo wa  madaraka  (separation  of  powers)  kati  ya  Utawala (executive), Bunge na Mahakama.

Madhumuni halisi ya mgawanyo huo ni kuzuia muhimili mmoja kuhodhi madaraka yote na hivyo kuwa na nguvu zaidi kuliko mhimili mwingine. 

Kila mhimili umepewa uwezo na mamlaka na maeneo ya kazi na pia kufanya kazi kwa kudhibiti mhimili mwingine kupitia dhana ya checks and balances. Katiba iko juu ya mihimili yote. Mgawanyo wa adaraka hapa Tanzania umegawanyika katika mihimili mitatu ambayo ni Bunge, Utawala/Serikali na Mahakama.  Ibara  ya  4  ya  Katiba  ya  Jamhuri  ya Muungano  wa  Tanzania  ya  mwaka  1997,  inaainisha  utekelezaji  wa shughuli za mamlaka ya nchi na kuzigawa katika mihimili hiyo mitatu na kusisitiza kila mhimili kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia masharti yaliyomo katika Katiba. 

 (ii) Uhuru wa Mahakama

Utawala wa sheria unahitaji uwepo wa mahakama huru katika utoaji haki.  Hii  ni  kutokana  na  ukweli  kuwa  mahakama  ndicho  chombo  chenye mamlaka na kauli ya mwisho ya utoaji wa haki nchini kulingana na masharti yaliyomo kwenye Ibara ya 107A ya Katiba. Mahakama katika kutoa uamuzi wa mashauri ya madai na jinai kwa kuzingatia sheria, mahakama zitafuata kanuni mahsusi zifuatazo kama zilivyotajwa katika Ibara ya 107A(2): 

a) Kutenda haki kwa wote bila kujali hali ya mtu kijamii au kiuchumi; 

b) Kutochelewesha haki bila sababu ya kimsingi; 

c) Kutoa fidia ipasavyo kwa watu wanaoathirika kutokana na Makosa ya watu wengine; na kwa mujibu wa sheria mahsusi iliyotungwa na Bunge; 

d) Kukuza na kuendeleza usuluhishi baina ya wanaohusika katika migogoro; 

e) Kutenda   haki   bila   kufungwa   kupita   kiasi   na   masharti   ya   kiufundi yanayoweza kukwamisha haki kutendeka. 

Aidha, Ibara ya 107B ya Katiba inaweka sharti kwamba katika kutekeleza majukumu  yake  ya  utoaji  haki,  mahakama  zote  ziko  huru  na  kwamba zinalazimika  kuzingatia  tu  masharti  ya  Katiba  na  sheria  za  nchi.  Kwa hiyo, Mahakama ni kiungo muhimu katika kulinda na kutetea utawala wa sheria.

(iii) Usawa wa watu mbele ya sheria 

Watu wote wana haki na wajibu sawa mbele ya sheria. Ubaguzi usio wa haki  kwa  misingi  ya  hadhi,  dini,  jinsia,  uanachama  kisiasa  au  rangi haukubaliki. Nguzo hii ya usawa wa watu mbele ya sheria imewekwa katika Ibara ya 13 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hivyo,  Mahakama  na  watekelezaji  wa  sheria  za  nchi  wanapaswa kuzingatia masharti hayo ya Katiba. 

(iv) Mchakato wa haki na haki za msingi (due process and natural law) 

Malengo ya mchakato wa haki ni kuhakikisha kuwa haki si tu inatendeka bali   ionekane   kwamba   imetendeka.   Mchakato   huo   huongeza uwezekano wa kufanya maamuzi sahihi kwa kufuata sheria. Mchakato wa  haki  unahusisha,  pamoja  na  mambo  mengine;  haki  za  kitawala kuongozwa na sheria; haki ya kusikilizwa; ; haki ya kufahamu mashtaka; haki ya kufahamu ushahidi unaohusika; haki ya kuwepo wakati shauri linasikilizwa  na  kuhoji  mashahidi  wanaotoa  ushahidi;  haki  ya  kujua sababu za maamuzi ya kiutawala au kimahakama; haki ya kukata rufaa au kuomba marejeo dhidi ya uaumuzi wa kiutawala au kimahakama.

 (v) Dhana ya kuchukuliwa kutokuwa na hatia (presumption of innocence) 

Kila mtu anadhaniwa kuwa hana hatia hadi inapothibitika vinginevyo kupitia mchakato wa haki (due process). Hivyo, hairuhusiwi na si haki kumnyoshea  kidole  kwa  kumhukumu  mtu  ambaye  shauri  dhidi  yake linachunguza na vyombo vya kiuchunguzi au kuendelea mahakamani kama inavyosisitizwa katika Ibara ya 13 (6)(b) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano   wa   Tanzania.  Vivyo   hivyo   kwa   mashauri   ambayo hayajafikishwa mahakamani au katika vyombo vya usalama wa Raia, wananchi hawapaswi kujichukulia  sheria  mkononi  kwa  kuwaadhibu wanaowatuhumu kwa uhalifu au kuanzisha fujo na uvunjifu wa amani na sheria kwa namna yoyote ile kwa madai ya kufuatilia haki zao. 

(vi) Kutoadhibiwa mara mbili (double jeopardy/res judicata) 

Mtu hawezi kuhukumiwa zaidi ya mara moja kwa kutenda kosa moja. Aidha,  katika  shauri  la madai,  suala  ambalo limetolewa  ufumbuzi  na mahakama  haliwezi  kufunguliwa  tena  mahakamani.  Nia hasa  ni kuhakikisha mashauri yanafikia tamati na kuepusha matumizi mabaya ya mchakato wa utoaji haki. 

 (vii)   Uhalali (Legality) 

Sheria sharti ziwe halali kwa maana ya kufuata masharti ya Katiba na ziwe zimetungwa kwa kufuata taratibu za utungwaji wa sheria zilizopo kama inavyoelezwa katika Ibara ya 64(5) ya Katiba yetu; 
“…..endapo  sheria  nyingine  yoyote  ikikiuka  masharti  yaliyomo katika Katiba hii, Katiba ndiyo itakuwa na nguvu, na sheria hiyo nyingine, kwa kiasi inachokiuka Katiba, itakuwa batili.” 

(viii)   Kueleweka (certainty) 

Utawala wa sheria unahitaji sheria ziwe rahisi ili zieleweke kwa wananchi walio    wengi    katika    kuzitekeleza.    Sheria    ambazo    hazieleweki zinaposomwa na  watumiaji  husababisha  haki  kutotendeka.  Ofisi  ya Mwanasheria  Mkuu  wa  Serikali  imekuwa  ikitimiza  jukumu  hili  kwa kuandika  miswada  ya  sheria  katika  lugha  na  mtindo  unaoiwezesha ieleweke  kwa  urahisi.  Na sasa  tumerasimisha  utaratibu  wa  kuandika sheria katika lugha mbili za Kiswahili na Kiingereza. 

Mhe. Rais, Nguzo hizo za utawala wa sheria zinaonyesha nafasi muhimu ya utawala wa sheria  katika  jamii.   Mbali  na  umuhimu  wake  katika  kukuza, demokrasia,  siasa,  haki  za  msingi  na  kuhakikisha  kuwa  Serikali inaongozwa  na sheria badala ya watu, utawala wa sheria una nafasi katika kukuza ustawi wa jamii na maendeleo ya uchumi. Kwa kweli ni vigumu jamii kuendelea kama jamii hiyo haizingatii   utawala wa sheria. 

Kwa upande mwingine, jamii ambayo ina mfumo mzuri unaoeleweka katika kutatua  migogoro  kama  ilivyo  hapa  kwetu  ambapo  Mahakama  ya  Tanzania imepewa mamlaka hayo, na migogoro katatuliwa kwa kufuata misingi ya sheria pasipokuwa  na  rushwa,  hongo  au  kishawishi  chochote  ikiwemo  vitendo  vya uvunjifu wa amani ni dhahiri kuwa ustawi wa uwekezaji, biashara, makampuni na wananchi utakua. Kama migogoro haiwezi kutatuliwa katika jamii kwa kufuata sheria, kuna hatari ya umoja na amani kutoweka na hivyo kudunisha maendeleo yetu.  Kwa msingi huo, mchango wa utawala wa sheria katika maendeleo ya jamii  kiuchumi  na  kisiasa    ni  muhimu  sana,  na  hivyo  kustahili  kuheshimiwa  na kuzingatiwa na kila mmoja wetu. 

Aidha, wanasheria wanayo nafasi kubwa katika utekelezaji wa wa utawala wa sheria. Kupitia wao wananchi hufikisha masuala yao mahakamani kwa ajili ya kusuluhishwa au kupatiwa ufumbuzi.   Kwa sababu hiyo tunalo jukumu na wajibu wa kuhakikisha kwamba matumizi ya taaluma yetu ya Uanasheria yanazingatia haja ya kudumishwa kwa matakwa ya Utawala wa Sheria ipasavyo. 

Mhe.  Rais,     Kama  nilivyotangulia  kusema,  uhuru  wa  mahakama  ambao umeanishwa  katika  Ibara  ya  107B  ya  Katiba  ya  Jamhuri  ya  Muungano  wa Tanzania, ni  nguzo muhimu ya utawala wa sheria. Uendeshaji wa Serikali kwa kufuata misingi ya kikatiba (constitutionalism) unakuwepo pale ambapo nchi ina mahakama ambayo ni huru na maamuzi yake hayaegemei upande wowote. Mahakama inakuwa huru pale inapoweza kutoa uamuzi wake bila shinikizo lolote la kimaslahi au ushawishi kutoka Serikalini, Bunge, watu binafsi ama taasisi yoyote kwa namna yoyote ile. 

Aidha, utovu wa maadili ya taaluma kwa Majaji, Wasajili, Mahakimu, Mawakili wa Serikali na Mawakili wa Kujitegemea unaweza kudhoofisha imani ya wananchi kwa mhimili huu muhimu. Jambo hili likitokea ni hatari sana kwa ustawi wa nchi yetu. Mahakama inatakiwa kuwa kimbilio la mtu anayeonewa au kudai haki ili kupata haki  yake.  Ndiyo maana  tunao  mfumo huru  wa kisheria ambao  watu hudai haki zao hata kama mdaiwa ni Serikali kama ambavyo tunavyoshuhudia kesi zikifunguliwa dhidi ya Serikali. 
Mhe. Rais, Mwisho napenda kutoa rai kwa wanasheria wenzangu kuendeleza mfumo wa uhuru wa taaluma ya sheria tulionao katika kutekeleza utawala wa sheria kwa kuzingatia yafuatayo;-

(i)  kufanya kazi kama maafisa wa mahakama,    kuwasilisha matakwa ya wateja kwa ukamilifu, uadilifu na kwa mujibu wa sheria, 

(ii) kulinda haki za watu   hata kama ni kundi chache (minority), ili mradi haki hizo zinatambuliwa katika msingi wa Katiba na Sheria za nchi yetu. 

(iii) kuanzisha mipango ya kuitaarifu jamii kuhusu haki na wajibu   wao   lakini bila kuhamasisha uasi dhidi ya mamlaka halali za Nchi; 

(iv) kuwezesha uelewa wa sheria kupatikana na kuwafikia wananchi katika muktadha au mtazamo sahihi wa kisheria na;-

(v) Kuelimisha wananchi watambue kwamba haki na uhuru wa binadamu ambavyo misingi yake imeorodheshwa katika Katiba yetu havitatumika na mtu mmoja kwa maana ambayo itasababisha    kuingiliwa kati au kukatizwa kwa haki na uhuru wa watu wengine au maslahi ya Umma. 

Mhe. Rais,   Mwaka 1994 katika Mkutano kuhusu Utawala wa Sheria na Vyombo vya Kikatiba (the Rule of Law and its Constitutional Organs) uliofanyika Windhoek Namibia ambapo Mheshimiwa Ismail Mohamed aliyekuwa Jaji Mkuu wa  Afrika  Kusini  na  Namibia  alisisitiza  ushiriki  wa  kila  mtu  katika  kuimarisha utawala wa sheria pale alipotamka; 

….to survive meaningfully, the values of the constitution and the rule of law must be emotionally internalised within the psyche of citizens. The active participation of the organs of civil society outside of the constitution in the articulation and dissemination of these values is a logistical necessity for the survival and perpetuation of the rule of law.” 

Inawezekana kuwa na taifa linalofuata msingi wa utawala wa sheria iwapo kila kila mtu atashiriki na kutimiza wajibu wake ipasavyo. 

Asanteni sana kwa kunisikiliza.

Sharing is Caring:


WE LOVE COMMENTS


Related Posts:

0 comments:

Post a Comment

Blog Archive

Followers